Salamu - Aprili, 2026

Bwana Yesu Kristo asifiwe. Tunamshukuru Mungu ametupa mwezi huu wa nne. Katika mwezi uliopita tumekuwa na semina kubwa mbili. Moja jijini Mbeya kwenye kanisa la Lutheran Bethania Mbalizi.

Na semina ya pili ni mkoani Songwe, kwenye kanisa la Moraviani Mbozi Mission. Tulikuwa na semina nzuri sana. Asanteni kwa maombi yenu.

Hebu tuanze kuzipokea salamu za mwezi huu. Kumbuka tuna salamu zenye kichwa:

JIFUNZE KUTAKA KARAMA AU KUOMBA MUNGU AKUPE KARAMA YA MIUJIZA NA UPONYAJI (SEHEMU YA PILI)

2: MUNGU HUTUMIA MUUJIZA ILI WATU WAMWAMINI MUNGU

Muujiza ni jambo lingine ambalo Mungu hulitumia ili watu wamwamini. Neno imani maana yake ni kuwa na uhakika. Sasa sikia, Mungu hutumia muujiza kama jambo la kuwafanya watu wawe na uhakika na Mungu.

Angalia mistari hii uone: “31 Israeli akaiona ile kazi kubwa aliyoifanya BWANA juu ya Wamisri, ndipo hao watu wakamcha BWANA, wakamwamini BWANA, na Musa mtumishi wake.” (Kutoka 14:31).

Angalia, muujiza ambao Mungu aliufanya siku ile ya kuikausha bahari ili wana wa Israeli wapite, Mungu aliutumia muujiza huo ili pia wamuamini.

Hao ndugu walipoona muujiza huo ambao Mungu aliufanya, wakajikuta wakijenga imani kwa Mungu.

Sikia unapoitaka karama ya miujiza, fahamu uutake kwa ajili ya watu hao kuongeza imani kwa Mungu. Angalia mistari hii mingine: “31 Na watu wengi katika mkutano wakamwamini; wakasema, Atakapokuja Kristo, je! Atafanya ishara nyingi zaidi kuliko hizi alizozifanya huyu?” (Yohana 7:31).

Kwa mujibu wa mistari hiyo unaona kuwa miujiza au ishara hutumika kuwafanya watu wasiomwamini Mungu waanze kuwa na imani kwa Mungu.

Angalia tena mfano huu mwingine uone: “12 Lakini walipomwamini Filipo, akizihubiri habari njema za ufalme wa Mungu, na jina lake Yesu Kristo, wakabatizwa, wanaume na wanawake. 13 Na yeye Simoni mwenyewe aliamini akabatizwa, akashikamana na Filipo; akashangaa alipoziona ishara na miujiza mikubwa inayotendeka. 14 Na mitume waliokuwako Yerusalemu, waliposikia ya kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu, wakawapelekea Petro na Yohana.” (Mdo 8:12–14).

Simoni mchawi alipoona miujiza aliyoifanya Mungu kwa kumtumia Filipo, akaanza kumwamini Mungu. Ina maana kama asingeona miujiza mikubwa ya Mungu, asingeweza kumwamini Mungu.

Sikia unapomuomba Mungu akupe karama ya miujiza, uwe na lengo la kuona miujiza ikiimarisha imani kwa Mungu.

Angalia mistari hii uone: “1 Musa akajibu akasema, Lakini, tazama, hawataniamini, wala hawataisikia sauti yangu; maana watasema, BWANA hakukutokea. 2 BWANA akamwambia, Ni nini hiyo uliyo nayo mkononi mwako? Akasema, Ni fimbo. 3 Akamwambia, Itupe chini; akaitupa chini, nayo ikawa nyoka; Musa akakimbia mbele yake. 4 BWANA akamwambia Musa, Nyosha mkono wako, kamshike mkia; (akaunyosha mkono wake akamshika, naye akageuka kuwa fimbo mkononi mwake;) 5 ili kwamba wapate kusadiki ya kwamba BWANA, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, Mungu wa Yakobo, amekutokea. 6 BWANA akamwambia tena, Sasa tia mkono wako kifuani mwako. Akautia mkono wake kifuani mwake; naye alipoutoa, kumbe! mkono wake ulikuwa na ukoma, umekuwa mweupe kama theluji. 7 Akasema, Tia mkono wako kifuani mwako tena. Akautia mkono wake kifuani mwake tena, na alipoutoa kifuani mwake, kumbe! umerudia hali ya mwili wake. 8 Basi itakuwa, wasipokusadiki, wala kuisikiliza sauti ya ishara ya kwanza, wataisikiliza sauti ya ishara ya pili. 9 Kisha itakuwa wasipoamini hata ishara hizo mbili, wala kuisikiliza sauti yako, basi, yatwae maji ya mtoni uyamwage juu ya nchi kavu, na yale maji uyatwaayo mtoni yatakuwa damu juu ya nchi kavu.” (Kutoka 4:1–9).

Miujiza aliyoifanya Mungu kwa kumtumia Musa na Haruni ilitumika huko Misri kuwajengea wana wa Israeli na Wamisri imani kwa Mungu.

Sikia, Wamisri na hata wana wa Israeli walikuwa hawana imani kwa Mungu wa mbinguni. Wamisri na hata wana wa Israeli walikuwa wana imani sana kwa miungu ya Wamisri. Ili wana wa Israeli na hata Wamisri waanze kujenga imani kwa Mungu, ni baada ya kuanza kuona miujiza mikubwa kutoka kwa Mungu.

Katika eneo hili pia unatakiwa ujifunze kuwa unaweza ukawa na karama ya miujiza lakini watu wakawa hawana imani na wewe na hata kwa Mungu. Ukilijua jambo hili, hautakuwa na wasiwasi.

Angalia na mistari hii: “36 Maadamu mnayo nuru, iaminini nuru hiyo, ili mpate kuwa wana wa nuru. Hayo aliyasema Yesu, akaenda zake, akajificha wasimwone. 37 Walakini ajapokuwa amefanya ishara nyingi namna hiyo mbele yao, hawakumwamini; 38 ili litimie lile neno la nabii Isaya alilolisema, Bwana, ni nani aliyezisadiki habari zetu? Na mkono wa Bwana amefunuliwa nani? 39 Ndiyo sababu wao hawakuweza kusadiki; kwa maana Isaya alisema tena, 40 Amewapofusha macho, ameifanya mizito mioyo yao; wasije wakaona kwa macho yao, wakafahamu kwa mioyo yao, wakaongoka, nikawaponya.” (Yohana 12:36–40).

Angalia na mistari hii: “30 Yule mtu akajibu, akawaambia, Hii ni ajabu! Kwamba ninyi hamjui atokako, naye alinifumbua macho! 31 Twajua ya kuwa Mungu hawasikii wenye dhambi; bali mtu akiwa ni mcha Mungu, na kuyafanya mapenzi yake, humsikia huyo. 32 Tokea hapo haijasikiwa ya kuwa mtu ameyafumbua macho ya kipofu, ambaye alizaliwa hali hiyo. 33 Kama huyo asingalitoka kwa Mungu, asingeweza kutenda neno lo lote. 34 Wakajibu, wakamwambia, Ama! Wewe ulizaliwa katika dhambi tupu, nawe unatufundisha sisi? Wakamtoa nje. 35 Yesu akasikia kwamba wamemtoa nje; naye alipomwona alisema, Wewe wamwamini Mwana wa Mungu? 36 Naye akajibu akasema, Ni nani, Bwana, nipate kumwamini? 37 Yesu akamwambia, Umemwona, naye anayesema nawe ndiye. 38 Akasema, Naamini, Bwana. Akamsujudia.” (Yohana 9:30–38).

Ukiisoma mistari hiyo unajifunza kuwa moja ya kazi ya miujiza ni kumfanya mtu au watu wamwamini Bwana Yesu Kristo.

Muujiza unaweza kutumika kuwafanya wasiomjua au kumwona Bwana Yesu Kristo wamuone na wamwamini.

Usizuie miujiza ya Mungu kwa sababu tu watu wasiamini. Sikia, si kila mtu ataamini; wapo watakaoamini, haijalishi ni wangapi.

Biblia inasema hivi: “13 Kama sisi hatuamini, yeye hudumu kuwa mwaminifu. Kwa maana hawezi kujikana mwenyewe.” (2 Timotheo 2:13).

Usiogope ikiwa Mungu amekupa karama ya miujiza na watu wakawa hawaamini. Wewe songa mbele, kwani hata wao wasipoamini, fahamu Mungu hudumu kuwa mwaminifu.

Naamini umenielewa. Tuonane katika eneo hili hili la salamu ya mwezi ujao.

Mungu akubariki sana.

Ukihitaji masomo yetu, unaweza kuyapata kwa njia zifuatazo:

1. App yetu ya huduma yenye jina “HUSONEMU (MWAKATWILA)” — inapatikana Play Store, ambapo kuna masomo mengi sana.

2. Tovuti yetu: www.mwakatwila.org

3. YouTube: HUDUMA YA SOMA NENO LA MUNGU

4. Facebook: ingia kwenye tovuti yetu uone alama ya Facebook (f), kisha “like” ili upate maelezo ya kujiunga, au tafuta “SOMA NENO LA MUNGU”

5. Instagram: tafuta “Huduma ya Soma Neno la Mungu”

6. DVDs 📀 au CDs 💿

7. Vitabu

NB: Wasiliana na mhudumu ofisini kwa namba +255 763 109 733 ili kupata vitabu, DVD na CD.

8. Kwa njia ya redio:

  • Rungwe FM 102.5 MHz — Jumapili saa 3:00 hadi 4:00 usiku
  • Baraka FM 107.7 MHz — Jumanne saa 12:00 jioni hadi 1:00 usiku
  • Bomba FM 104.1 MHz — Ijumaa saa 3:00 hadi 4:00 usiku

9. Online Radio: radio.mwakatwila.org

Ratiba ya vipindi:

  • Saa 12:00 asubuhi
  • Saa 07:00 mchana
  • Saa 12:00 jioni
  • Saa 03:00 usiku

10. Ingia MWAKATWILA YouTube Online

Kwa mawasiliano zaidi:

+255 754 849 924
+255 756 715 222

Wako,
Mwl. Steven Mwakatwila & Beth Mwakatwila